Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru, Mheshimiwa Seif Dauda, leo Jumatano tarehe 4 Februari 2026, ameongoza kikao maalum cha pamoja na wazee wa Wilaya ya Tunduru kilichofanyika katika ukumbi wa Halmashauri. Kikao hicho kililenga kujadili masuala mbalimbali yanayohusu maendeleo ya wilaya pamoja na ustawi wa jamii kwa ujumla.

Pichani:Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru, Mhe. Seif Dauda
Katika kikao hicho, wajumbe walipata fursa ya kujadili kwa kina changamoto zinazowakabili wananchi wa Wilaya ya Tunduru, zikiwemo upatikanaji wa maji safi na salama, huduma za afya, umeme, miundombinu ya barabara pamoja na usalama wa raia.
Mhe.Dauda alisisitiza kuwa wazee ni nguzo muhimu ya maendeleo katika Wilaya ya Tunduru. Alieleza kuwa kuwepo kwa ushirikiano wa karibu kati ya uongozi na wazee kutasaidia kutatua changamoto kwa urahisi na kwa wakati. Hivyo, aliwahimiza wadau wote kuimarisha mshikamano, ushirikiano na mawasiliano ya karibu ili kuhakikisha maendeleo endelevu yanapatikana kwa manufaa ya wananchi wote wa Wilaya ya Tunduru.

Pichani:Baadhi ya Wazee walaya ya Tunduru.
Akitolea ufafanuzi kuhusu changamoto zilizowasilishwa na wazee, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru, Ndugu Chiza Marando, alieleza kuwa Halmashauri itahakikisha changamoto zote zilizobainishwa zinafanyiwa kazi kwa kushirikiana na taasisi husika. Pia aliahidi kuzingatia na kufanyia kazi ushauri uliotolewa na wazee hao, sambamba na kuendeleza na kudumisha uhusiano mzuri kati ya wazee na uongozi wa Halmashauri.
Aidha, kikao hicho kilijadili mikakati ya kuimarisha ushirikiano kati ya uongozi wa Halmashauri na wazee katika kusimamia, kushauri na kusukuma mbele ajenda za maendeleo na kijamii ndani ya wilaya.
Halmashauri ya Wilaya Tunduru
Anuani ya Posta: 275, TUNDURU
Simu: + 255-025-2680004
Simu ya Nununu:
Barua Pepe: info@tundurudc.go.tz
Hakimiliki©2019 Halmashauri ya Wilaya Tunduru.Haki zote zimehifadhiwa.