Mji wa Tunduru umeandika historia mpya katika juhudi za kuhakikisha upatikanaji wa majisafi kwa wakazi wake kufuatia hafla ya kihistoria ya utiaji saini mkataba wa mradi kabambe. Mradi huu wenye thamani kubwa ya zaidi ya shilingi bilioni 3.2 unalenga kuleta mageuzi makubwa katika huduma ya maji na kukomesha tatizo la uhaba kwa muda mrefu.
Hafla hiyo muhimu iliyoshuhudiwa na Mkuu wa Wilaya ya Tunduru Mhe. Simon Chacha na viongozi mbalimbali wa serikali, uongozi wa Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru na Mamlaka ya Maji na Usafi wa Mazingira Tunduru (TUUWASA), inatoa matumaini kwa wananchi wa Tunduru kuwa sasa wanaelekea kwenye uhakika wa maji kwa kipindi cha takriban miongo miwili ijayo. Utiaji saini huu unaashiria mwanzo wa safari itakayoboresha maisha ya maelfu ya watu na kuchochea maendeleo endelevu katika wilaya hiyo.
Akizungumza katika hafla hiyo Mhe. Simon Chacha, alieleza kuwa mradi huu ni kielelezo cha dhamira ya serikali katika kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora na endelevu ya majisafi. Alisisitiza kuwa upatikanaji wa maji ni msingi muhimu kwa maendeleo ya kiuchumi na kijamii. Vilevile alizisisitiza kampuni hizo zilizotia saini ya kutekeleza mradi huo juu ya kuhakikisha unakamilika kwa muda na viwango vilivyokusudiwa na Wizara ya Maji.
"Utiaji saini wa mkataba huu ni hatua kubwa sana kwa wananchi wa Tunduru," alizungumza Mhe. Chacha "Mradi huu wa Zaidi ya bilioni 3.2 siyo tu utaongeza upatikanaji wa maji, bali pia utaboresha miundombinu yote ya usambazaji, kuhakikisha maji safi na salama yanawafikia wananchi kwa uhakika kwa miaka mingi ijayo."
Mkurugenzi wa TUUWASA Mhandisi.Cuthbert Richard Kiwia alielezea kwa kina kuhusu mradi huo, akifafanua kuwa utahusisha ujenzi wa tenki la maji lenye ujazo wa Lita milioni 1, tenki la kwenda juu lenye urefu wa mita 6, ununuzi na uongezaji wa mabomba, ujenzi wa tegeo la maji kwenye mto Nanjoka, ununuzi na ufangaji wa pampu 7, ununuzi wa gari, ujenzi wa kisima cha pampu, ujenzi wa ofisi pamoja na ununuzi wa thamani zake. Mradi huu utagharimu kiasi cha shilingi Bilioni 3,261,177,554.26 bila ongezeko la kodi.
“Mradi huu utakapokamilika utakuwa na uwezo wa kuzalisha maji lita millioni 8,283,224, kutoka lita milioni 3.7 ambayo inazalishwa kwa sasa, huduma ya maji itaongezeka kutoka asilimia 78 hadi 100, Zaidi ya wananchi wapatao elf 60 watanufaika, vijiji 20 vitanufaika na mradi huu moja kwa moja, vijiji hivyo ikiwa ni Ujenzi, Exitended, Kalonga, Nakayaya Mashariki, Tuleane, Mkwanda, Majengo, Kalanje, TANESCO, Biasi, Kalonga, Mkwanda, Lambai, Masonya, Ngalinje, Mchangani, Muungano, Nanjoka, National House”. Alibainisha Mhandisi. Kiwia
Mhandisi.Cuthbert Richard Kiwia aliendelea kutoa ufafanuzi kuwa ili mradi huu ukamilike kwa ufanisi na kwa muda uliopangwa, kazi hizo ziligawanywa katika kampuni tatu tofauti, ambapo, zabuni ilitangazwa kupitia mfumo wa manunuzi wa serikali (Nest), kampuni hizo zilizoshinda na kupitishwa na bodi ya wazabuni alizitaja kuwa ni one nagg group limited ambaye amesaini mkataba wa shilingi Bilioni 2.1, AKWIJA multake Limited amesaini mkataba wa Milioni 147, Plasco Limited billioni 1.1.
Aidha Mkuu wa Wilaya ya Tunduru, Mheshimiwa Chacha alimpongeza pia Mkurugenzi wa Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Mjini Tunduru (TUUWASA) Mhandisi.Cuthbert Richard Kiwia kwa kazi nzuri anayoifanya, akibainisha kuwa hakujakuwa na malalamiko yoyote hadi sasa, na mipango mipya kabambe ya kuboresha huduma inaendelea kuandaliwa kwa manufaa ya wananchi.
Inatarajiwa kuwa utekelezaji wa mradi huu utaanza hivi karibuni, na utakapokamilika, utakuwa na manufaa makubwa kwa wakazi wa Tunduru kwa kuhakikisha upatikanaji wa majisafi kwa matumizi ya nyumbani, biashara, na shughuli nyingine za kijamii na kiuchumi kwa zaidi ya miongo miwili ijayo.
Halmashauri ya Wilaya Tunduru
Anuani ya Posta: 275, TUNDURU
Simu: + 255-025-2680004
Simu ya Nununu:
Barua Pepe: info@tundurudc.go.tz
Hakimiliki©2019 Halmashauri ya Wilaya Tunduru.Haki zote zimehifadhiwa.