Wilaya ya Tunduru imepiga hatua muhimu katika kuimarisha ulinzi, usalama na utoaji wa haki katika masuala ya jinsia na watoto kufuatia uzinduzi rasmi wa jengo la Dawati la Jinsia na Watoto, uliofanyika leo tarehe 09 Februari, 2026.
Jengo hilo limezinduliwa na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Ruvuma, SACP Marko Chilya, ambaye amesema kuwa uwepo wa jengo hilo utarahisisha utoaji wa huduma za kisheria, ushauri na ulinzi kwa waathirika wa vitendo vya ukatili wa kijinsia na unyanyasaji dhidi ya watoto katika Wilaya ya Tunduru.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, SACP Marko Chilya amesisitiza umuhimu wa jamii kushirikiana na Jeshi la Polisi katika kupinga vitendo vya ukatili, huku akibainisha kuwa Dawati la Jinsia na Watoto ni nyenzo muhimu ya kuhakikisha haki, usalama na ustawi wa makundi maalum yanalindwa ipasavyo.
Tukio hilo lilipambwa na watoto kutoka katika Shule za Msingi na awali za wilayani Tunduru, Aidha,watoto kutoka Kituo cha Malezi ya Watoto Wadogo Mchana "Bright Future" walikua kivutio , ambapo walionesha ujumbe mbalimbali kupitia mabango yenye kaulimbiu zinazoelezea umuhimu wa uwepo wa Dawati la Jinsia na Watoto katika jamii, hatua iliyovutia hisia za washiriki wa hafla hiyo.


Uzinduzi wa jengo hilo unaonesha dhamira ya Serikali kupitia Jeshi la Polisi katika kuimarisha mazingira salama kwa wananchi wote, pamoja na kuhakikisha haki zao zinalindwa kwa vitendo, sambamba na malengo ya Taifa ya kutokomeza ukatili wa kijinsia na unyanyasaji.
Halmashauri ya Wilaya Tunduru
Anuani ya Posta: 275, TUNDURU
Simu: + 255-025-2680004
Simu ya Nununu:
Barua Pepe: info@tundurudc.go.tz
Hakimiliki©2019 Halmashauri ya Wilaya Tunduru.Haki zote zimehifadhiwa.