Wananchi wa Nandembo wamepatiwa elimu kuhusu umuhimu wa Amani, Upendo na Mshikamano katika kushiriki na kuendesha shughuli mbalimbali za kijamii, ikiwa ni pamoja na misiba, harusi na michezo, ili kuimarisha mahusiano mema na mshikamano ndani ya jamii.
Elimu hiyo ilitolewa na viongozi wa Jukwaa la Viongozi wa Dini Wilaya ya Tunduru, wakiongozwa na Mchungaji Emmanuel Kanduru, Mwenyekiti wa Jukwaa hilo, pamoja na Shekhe Zuberi Mnandi, Katibu wa Jukwaa la Viongozi wa Dini Tunduru. Viongozi hao walisisitiza umuhimu wa ushirikiano miongoni mwa wanajamii bila kujali tofauti za kidini, wakieleza kuwa amani na mshikamano ni msingi wa maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Aidha, sambamba na utoaji wa elimu hiyo, wananchi wa Nandembo walipata fursa ya kushiriki michezo mbalimbali ikiwemo mpira wa miguu (draft) na mchezo wa bao, ikiwa ni sehemu ya kuimarisha mshikamano na kuleta jamii pamoja katika mazingira ya amani na furaha.
Kupitia udhamini wa Shirika la FPCT-STCC, linalotekeleza Mradi wa Kuimarisha Amani, Upendo na Mshikamano kwa waumini wa madhehebu mbalimbali ya dini, washindi wa michezo hiyo walipatiwa zawadi. Mshindi wa mchezo wa mpira wa miguu alipatiwa jezi, huku mshindi wa pili akipatiwa mpira, ili kuendelea kuendeleza shughuli zao za kimichezo.

Tukio hili limeonesha kwa vitendo namna Serikali, taasisi za kidini na vikundi vya wanajamii, ikiwemo timu za michezo, vinavyoweza kushirikiana katika kuleta wananchi pamoja, kutoa elimu kwa jamii na kuchochea mabadiliko chanya yanayojenga mshikamano na amani ya kudumu katika jamii.
Halmashauri ya Wilaya Tunduru
Anuani ya Posta: 275, TUNDURU
Simu: + 255-025-2680004
Simu ya Nununu:
Barua Pepe: info@tundurudc.go.tz
Hakimiliki©2019 Halmashauri ya Wilaya Tunduru.Haki zote zimehifadhiwa.