Mafunzo maalum yaliyolenga kuwajengea uwezo Local fundi, makundi maalum pamoja na wazabuni yamefanyika leo ,tarehe 07/02 katika ukumbi wa Klasta-Mlingoti, kwa lengo la kuwawezesha kutumia kwa ufanisi Mfumo wa Kitaifa wa Ununuzi wa Umma kwa Njia ya Kielektroniki (NEST) wakati wa kuomba na kushiriki zabuni za Serikali.

Mafunzo haya maalum, yameandaliwa na Mamlaka ya Kudhibiti Ununuzi wa Umma (PPRA) na Ofisi ya Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru kupitia Kitengo cha Umamizi wa Ununuzi na Ugavi , yamehusisha pia Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) waliokaribishwa kutoa elimu maalum kwa washiriki.
Ndg. Theophil Ngowi, Afisa Ununuzi kutoka PPRA, ameeleza kuwa lengo kuu la mafunzo ni kuongeza uelewa, ushiriki na ushindani wa haki kwa wazabuni wa ndani, sambamba na kupunguza changamoto zinazowakabili wakati wa matumizi ya mfumo wa NEST.

Washiriki wamepatiwa mafunzo ya kina kuhusu, Fursa zinazopatikana kwenye upendeleo wa makundi maalumu, hatua za kujiandikisha, kuomba zabuni na kufuatilia taarifa mbalimbali katika NEST, pamoja na sheria, kanuni na taratibu zinazowalinda wanaposhiriki zabuni, hatua itakayosaidia kuongeza uwazi, haki na uaminifu katika mchakato wa manunuzi ya umma.
Washiriki wameeleza kuridhishwa na elimu waliyoipata, wakibainisha kuwa itawasaidia kujiamini zaidi kushiriki zabuni za Serikali, kuboresha usimamizi wa biashara zao na kunufaika kikamilifu na fursa za kiuchumi.

Mafunzo haya ni sehemu ya jitihada za Serikali na PPRA za kuwajengea uwezo mafundi wa ndani, makundi maalum na wazabuni, ili kuhakikisha wanashiriki kikamilifu katika miradi na zabuni za Serikali, na kuchochea ukuaji wa uchumi wa ndani na maendeleo endelevu ya jamii.
Halmashauri ya Wilaya Tunduru
Anuani ya Posta: 275, TUNDURU
Simu: + 255-025-2680004
Simu ya Nununu:
Barua Pepe: info@tundurudc.go.tz
Hakimiliki©2019 Halmashauri ya Wilaya Tunduru.Haki zote zimehifadhiwa.