Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru imeendelea na ziara maalum za kutembelea vijiwe vya maafisa usafirishaji wa bodaboda, bajaji na maguta katika maeneo mbalimbali ya wilaya hiyo, ikiwa ni mwendelezo wa juhudi za Serikali za kuwafikia vijana moja kwa moja katika maeneo yao ya kazi, kuwapatia elimu, kusikiliza changamoto zao na kuwaunganisha na fursa mbalimbali za maendeleo.

Katika ziara hizo, wataalamu walitoa elimu kuhusu fursa za kiuchumi zilizopo ndani ya Wilaya ya Tunduru, ikiwemo mikopo ya asilimia 10 inayotolewa na Halmashauri kwa vikundi vya vijana, wanawake na watu wenye ulemavu, pamoja na fursa za mikopo ya vyombo vya moto kama pikipiki, bajaji na maguta inayotolewa na Benki za NMB na CRDB, kwa lengo la kuwawezesha vijana kumiliki vyombo vyao na kujitegemea kiuchumi.
Aidha, vijana walipatiwa taarifa kuhusu fursa za mafunzo ya muda mfupi ya udereva yatakayokuwa yakitolewa na Chuo cha Ufundi Nazareth Mbesa – Tawi la Tunduru Mjini (Biasi). Mafunzo hayo yanalenga kuwawezesha vijana kupata vyeti vya mafunzo ya udereva na kumiliki leseni halali, hatua itakayowawezesha kufanya kazi kama madereva rasmi wanaotambulika kwa mujibu wa sheria.

Katika kutekeleza adhma ya Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, ya kuwafikia na kuwasikiliza vijana, viongozi na wataalamu wa Halmashauri walisikiliza na kupokea changamoto pamoja na ushauri uliotolewa na vijana, ili kuzifanyia kazi na kuboresha mazingira yao ya kazi na maisha kwa ujumla.
Vilevile, elimu ilitolewa kuhusu huduma ya msaada wa kisheria kupitia Kampeni ya Mama Samia Legal Aid Campaign, inayotolewa bila malipo kwa wananchi, kwa lengo la kutatua migogoro katika jamii, kulinda haki za wananchi na kuwezesha maendeleo endelevu.
Katika ziara hizo, vijana pia walielimishwa kuhusu umuhimu wa kudumisha amani, upendo na mshikamano katika jamii, hususan kwa makundi ya watoa huduma za usafirishaji, ili kuhakikisha usalama, utulivu na maendeleo ya Wilaya ya Tunduru vinaendelea kudumishwa wakati wote.
Ziara hizi ni sehemu ya mpango endelevu wa Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru wa kuendelea kutembelea vijiwe vya bodaboda, bajaji na maguta, kama mkakati wa Serikali wa kuwafikia vijana moja kwa moja, kutatua changamoto zao na kuwawezesha kushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo ya kiuchumi na kijamii, kwa ustawi wa vijana na maendeleo ya wilaya kwa ujumla.
Halmashauri ya Wilaya Tunduru
Anuani ya Posta: 275, TUNDURU
Simu: + 255-025-2680004
Simu ya Nununu:
Barua Pepe: info@tundurudc.go.tz
Hakimiliki©2019 Halmashauri ya Wilaya Tunduru.Haki zote zimehifadhiwa.