Zoezi la uhamasishaji, uelimishaji na uchangiaji wa damu ni zoezi endelevu linalolenga kuokoa maisha ya wahitaji na kuhakikisha upatikanaji wa damu salama katika vituo vyote vya kutolea huduma za afya. Kupitia zoezi hili, Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru imeendelea kufika katika maeneo mbalimbali ikiwemo shule, makanisa na misikiti ili kutoa elimu kwa jamii kuhusu umuhimu wa uchangiaji wa damu.

Kwa kipindi cha kuanzia tarehe 02 hadi 06 Februari, 2026, Idara ya Afya ya Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru, kwa kushirikiana na Timu ya Damu Salama Kanda ya Kusini kutoka Mtwara, ilifanikiwa kutekeleza zoezi la kuelimisha, kuhamasisha na kukusanya damu kupitia shule za sekondari zilizopo wilayani humo.
Shule zilizoshiriki katika zoezi hilo ni pamoja na Shule ya Sekondari Tunduru, Semeni, Lukumbule, Shule ya Sekondari ya Wasichana Masonya, Mataka pamoja na Shule ya Sekondari Frankweston. Kupitia ushiriki mzuri wa wanafunzi na walimu, jumla ya chupa 224 za damu salama zilikusanywa.

Zoezi hili lina lengo la kuhakikisha wagonjwa wote wenye uhitaji wa damu wanapata huduma kwa wakati, pamoja na kuimarisha upatikanaji wa damu salama katika vituo vyote vya kutolea huduma za afya wilayani Tunduru.
Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru inaendelea kuhimiza jamii kushiriki kikamilifu katika uchangiaji wa damu, kwa kuwa damu salama ni faraja na uhai kwa wagonjwa.
Halmashauri ya Wilaya Tunduru
Anuani ya Posta: 275, TUNDURU
Simu: + 255-025-2680004
Simu ya Nununu:
Barua Pepe: info@tundurudc.go.tz
Hakimiliki©2019 Halmashauri ya Wilaya Tunduru.Haki zote zimehifadhiwa.